Labels

Wednesday, July 15, 2015

MGAWANYO WA TANZU NA VIPERA VYA FASIHI SIMULIZI.

Katika makala hii tunaanza na kuelezea maana ya fasihi, fasihi fasihi simulizi kwa kutumia wataalam mbalimbali, baada ya kuelewa vizuri dhana hizi tutajadili vigezo vilivyotumika katika mgawanyo wa tanzu na vipera vya fasihi simulizi katika makala ya M.M Mulokozi (1989) na hatimaye tutaangalia ubora na udhaifu wa uainishaji wa tanzu hizo, na kumalizia na hitimisho, kielelezo na mwisho marejeo.
Fasihi ni sanaa itumiayo lugha ili kufikisha ujumbe kwa jamii bila kujali kuwa imeandikwa au haijaandikwa. Fasihi ambayo haijaandikwa ni fasihi simulizi na fasihi iliyoandikwa ni fasihi andishi.
Ama kuhusu Fasihi simulizi, Wamitila ( 2002) anaeleza kuwa Fasihi simulizi ni fasihi ambayo huwasilishwa kwa njia ya mdomo kwa kusimuliwa, kuimbwa , kutongolewa au kughanwa.
Naye Mulokozi (1996) anaelezea kuwa fasihi simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa njia ya mdomo na vitendo bila maandalizi.
Kwa ujumla fasihi simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa njia ya masimulizi  ya mdomo na vitendo bila maandishi.
Katika makala ya M.M Mlokozi (1989) katika mulika ya 21 amejaribu kuzigawa tanzu za fasihi simulizi ya Tanzania katika tanzu zake mahususi kwa kuzingatia VIGEZO vifuatavyo;
Umbile na tabia ya kazi inayohusika;upande wa umbile na tabia ya kazi ya sanaa ameangalia vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa na kuipa mwelekeo au mwenendo ilionao.Vipengele hivyo ni namna lugha inavyotumika(kishairi,kinathali,kimafumbo,kiwimbo, kighani nakadharika) pia muundo wa fani hiyo na wahusika kama wapo.
Kigezo cha pili ni muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira (hili linazingatia pia dhima yake kijamii) hapa Mulokozi amezingatia ukweli wa msingi kuwa fasihi simulizi ni sanaa inayo pita, isiyofungwa katika umbo maalum, wala matini maalum yasiyo badilika. Fasihi simulizi inatawaliwa na vitu muhimu vitatu yaani watu, wakati na mahali. Mwingiliano huu ndio muktadha, na muktadha ndio unaamua fani fulani ya fasihi simulizi ichukue umbo lipi? Iwasilishe vipi kwa hadhira, kwenye wakati na mahali hapo.

Zifuatazo ni tanzu na vipera vya fasihi simulizi kama zilivyoainishwa na M.M.Mlokozi(1989) katika mulika 21 na jinsi alivyo ziainisha kwa kutumia vigezo hivi viwili, yaani kigezo cha umbile na tabia ya kazi inayohusika na kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishwaji kwa hadhira, na vipera vyake.
M.M.Mulokozi ameainisha tanzu sita ambazo ni; mazungumzo, masimulizi, maigizo (drama) ushairi semi na ngomezi (ngoma).Hivyo ufuatao ni uainishaji wa tanzu hizi za fasihi simulizi na vipera vyake kwa kutumia vigezo vya Mulokozi katika mulika ya 21.
Mazungumzo, ni maongezi au maelezo ya mdomo katika lugha ya kawaida, juu ya jambo lolote lile. Si kila mazungumzo ni fasihi mazungumzo ili yawe fasihi lazima yawe na usanii wa aina fulani, na uhalisia baada ya kuunakili.
Tanzu zinazoingia katika fungu la mazungumzo; Hotuba, Malumbano ya watani, Ulumbu, Soga na mawaidha. Katika kuainisha tanzu hizi ndani ya mazungumzo M.M.  Mulokozi ametumia vigezo vyote viwili; Hotuba, malumbano ya watani, ulumbu, soga na mawaidha. Kwa kuzingatia kigezo cha kwanza kinachozingatia msingi wa umbile na kazi inayohusika, tunaona tanzu hizi zote zina vipengele vya vinvyoumba sanaa na kuipa muelekeo au mwenendo ulionao, katika hotuba, malumbano ya watani, ulumbu, soga na mawaidha vyote vinavipegele vyake. Pia tanzu hizo zote zina maana ya lugha inayotumika. Mfano katika hotuba lugha rasmi ndiyo inayotumika, katika malumbano ya watani lugha ya kejeli mara nyingi ndio hutumika zaidi, mawaidha hutumia lugha rasmi au lugha za kikabila hutumika.
Pia katika kigezo umbile na tabia ya kazi inayohusika,katika kuainisha tanzu hizi mulokozi ametumia muundo wa fani na wahusika kama wapo.Tanzu zote hizo katika mazungumzo zina fani yake. Mfano katika malumbano ya watani ni tanzu inayozingatia fani zifuatazo; Kuna utani wa mababu, mabibi na wajukuu, utani wa mashemeji, utani wa kikabila na utanu wa marafiki. Kila kimojawapo kati ya fani hazi huwa na kanuni zake, miktadha yake na mipaka yake katika jamii zinazohusika.
Pia katika kuanisha tanzu za mazungumzo Mulokozi ametumia kigezo chake cha pili yaani kigezo kinachozingatia muktadha na namna ya uwasilishwaji wake kwa hadhira hili linazingatia pia dhima yake katika jamii kama ifuatavyo;

Ndani ya mazungumzo kuna hotuba, mawaidha, ulumbu, malumbano ya watani, soga; Tanzu hizi zote zinazingatia msingi wa fasihi kuwa ni sanaa inayopita, isiyofungiwa katika umbo maalum, wala matini yasiyobadilika. Mfano Hotuba ni sanaa inayopita, isiyofungwa katika umbo maaluma na matini yake hubadilika kulingana na matukio kama vile; matukio ya kidini, sherehe na kadharika. Hotuba hufuata wakati, watu na mahali. Katika kigezo hiki kinachozingatia muktadha na namna ya uwasilishwaji wake kwa hadhira huzingatia wakati, watu na mahali.Tunaona katika mazungumzo na tanzu zake zinazingatia wakati watu na mahali, mfano mawaidha huzingatia watu gani,wana umri gani, je ni vijana wa kiume au wa kike. Pia huzingatia mahali yaani tukio linapofanyika, mfano sebuleani au chumbani na pia wakati gani asubuhi, mchana au jioni.
Tanzu ya mazungumzo kwa ujumla imeainishwa kwa kutumia vigezo vyote viwili yaani kigezo cha umbile na tabia ya kazi inayohusika na kigezo kinachozingatia muktadha na namna ya uwasilishwaji wake kwa hadhira.
Masimulizi; ni fasihi yenye kusimulia habari  fulani.  Mulokozi (1989) anasema kuwa masimulizi ni fasihi ya kihadithi na fani zake huwa na sifa zifuatazo; hueleza atukio katika mpangilio fulani mahsusi, huwa na wahusika yaani watendaji au watendwaji katika matukio yanayosimulia, hutumia lugha ya kimaelezo, utambaji wake au utoaji wake huweza kuambatana na vitendo au ishara, na huwa na maudhui ya kweli au ya kubuni na yenye mafunzo fulani katika jamii.

Katika mulika 21 Mulokozi amegawanya masimulizi katika tanzu zifuatazo; za kihadithi na Tanzu za Kisalua.
Katika tanzu za kihadithi amezigawa katika makundi yafuatayo;
Ngano  ni hadithi za kimapokeo zitumizo wahusika kama wanyama,miti na watu kuelezea au kuonya kuhusu maisha.Utanzu huu unajumuisha fani kadhaa kama vile; istiara,mbazi,na kisa.
Tanzu za kisalua zimegawanywa katika fani zifuatazo; visakale, tarihi, visasili,. Hivyo tunaona kuwa katika uainishaji wa tanzu hii ya masimulizi mulokozi ametumia vigezo vyote viwili kama ifuatavyo; katika msingi wa umbile na tabia ya kazi inayohusika Mulokozi ameonyesha vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa na kuipa mwenendo ulionao. Na vipengele hivyo ni kama; lugha ya kimaelezo, maudhui, matukio na wahusika.Pia ameonyesha namna lugha inavyotumika mfano. Ngano hutumia lugha ya kimaelezo na visakale, mapisi, tarihi, kumbukumbu na visasili. Vipera hivi vyote hutumia lugha ya kimaelezo.
Pia katika msingi wa umbile na kazi inayohusika, kigezo hiki huzingatia muundo wa fani na wahusika kama wapo.Tanzu ya masimulizi ina fani zifuatazo kutokana na Mulokozi. Hueleza matukio katika mpangilio fulani mahususi, huwa na wahusika yaani watendaji au watendwaji katika matukio yanayosimuliwa, utambaji au utoaji wake huweza kuambatana na vitendo au ishara, huwa na maudhui ya kweli au ya kubuni na yenye mafunzo fulani na hutumia lugha ya kimaelezo.   
Semi ni tungo au kauli fupifupi zenye kubeba maana fulani au mafunzo muhimu katika jamii, Mulokozi ameaimisha tanzu za semi kama ifuatavyo:-
Methali ni semi fupi fupi zenye kueleza kwa muhtasari fikra au mafunzo mazito yaliyotokana na uzoefu wa jamii. Methali huwa na sehemu mbili kwanza sehemu ambayo huanzisha wazo fulani sehemu ya pili ambayo hulikanusha au kulikamilisha wazo hilo. Methali ni utanzu tegemezi ambao kutokea kwake hutegemea fani nyingine mfano maongezi, majadiliano mazito, muktadha maalum katika methali Mulokozi ameainisha tanzu hii kwa kutumia kigezo cha umbile na tabia ya kazi inayohusika, katika kigezo hiki Mulokozi ameonyesha matumizi ya lugha. Mfano methali hutumia tamathali, sitiari na mafumbo. Pia methali huwa na wahusika wa fani zake zinazojitegemea. Mfano Haraka haraka / Haina Baraka. Wahusika kuna anayeuliza Haraka haraka na anayejibu Haina Baraka. Pia lugha aliyotumia katika methali hii ni lugha ya kinathari na kishairi.

Pia methali huwa na fani zake. Mulokozi anasema methali ni utanzu tegemezi ambao kutokea kwake hutegemea fani nyingine, fani hizo ni maongezi au majadiliano mazito, muktadha maalumu, huwa na sehemu mbili sehemu ya kwanza ambayo huanzisha wazo fulani na sehemu ya pili ambayo hulikamilisha au kukanusha wazo hilo.
Ndani ya kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishaji methali huwa na dhima ya kutoa mafunzo, kuadibisha, kuonya na kuhamasisha jamii. Methali huendana na wakati, watu na mahali kwa kuzingatia tukio pia huwa na matini yanayobadilika. Mfano Haraka haraka haina Baraka, methali hii inatoa onyo kuwa ukifanya jambo kwa haraka unaweza kukosea, hivyo polepole ndio mwendo.
Vitendawili; hizi ni usemi uliofumbwa ambao hutolewa kwa hadhira ili waifumbue. Fumbo hilo kwa kawaida huwa linafahamika katika jamii hiyo na mara nyingi lina mafunzo muhimu kwa washiriki mbali na kuwachemsha akili zao.  Vitendawili hutegemea uwezo wa kutambua, kuhusisha na kulinganisha vitu vya aina mbalimbali vilivyomo katika maumbile, ni sanaa inayojitegemea, inayotendwa na ina jisimamia yenyewe.
Katika kigezo cha umbile na tabia inayohusika vitendawili hutumia lugha ya mafumbo na huwa na washiriki yaani wahusika ambao ni yule anayetoa kitendawili na anayejibu. Mfano  Mmoja huulizaKitenawili na mwingine anajibu tega. Mfano; Kaa huku na mimi ni kae kule tumfinye mchawi (kula ugali), Mfano huu huhamasisha ushirikiano baina ya watu.
Pia vitendawili huwa na fani kama wahusika (pande mbili) wanaouliza na wanaojibu, muktadha maalumu (mazingira) katika muktadha na namna ya uwasilishaji Mulokozi amesema vitendawili huwa na mafunzo fulani zaidi ya chemsha bongo. Vitendawili huzingatia mazingira (mahali) watu na wakati maalum mfano watoto, mahali (shuleni au nyumbani) na huwa na wakati maalum.
Misimu, ni semi za muda na mahali maalum ambazo huzuka na kutoweka kutegemea mazingira maalum. Msimu ukipata mashiko ya kutosha katika jamii hatimaye huingia katika kundi la methali za jamii hiyo. Mfano  Tamu tamu mahonda ukinila utakonda.

Katika kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira misimu ni sanaa inayopita isiyofungiwa katika umbo maalum wala matini maalum yasiyobadilika. Misimu ina dhima ya kutoa mafunzo, kuonya, hutumika katika siasa pia misimu huenda na wakati, watu na mahali. Mfano Matteru (1987) anasema ‘tamu tamu mahonda ukinila utakonda’ . Katika  mfano huu unaonyesha madhara ya pombe iliyokuwa inatengenezwa na kiwanda cha mahonda (Zanzibar). Katika kigezo cha umbile na tabia ya kazi inayohusika misimu hutumia lugha isiyosanifu kwani huzuka na kutoweka mfano; mdebwedo, utajiju, yeboyebo,  buzi na kimeo.
Mafumbo ni semi za maonyo au mawaidha ambazo maana zake ni za ndani na zimefichika. Fumbo hubuniwa na msemaji kwa shabaha na hadhira maalum hivyo ni tofauti na methali ambazo ni semi za kimapokeo. Katika kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishwaji mafumbo huwa na dhima ya kutoa maonyo na mawaidha kwa jamii kwani hubuniwa kwa hadhira maalum. Mfano  ‘Mbele ya bata kuna bata na nyuma ya bata kuna bata, jumla nina bata wangapi’? Fumbo hili huonyesha umakini katika katika kufanya kitu. Katika mafumbo ndani ya kigezo cha umbile na tabia ya kazi inayohisika huangalia namna lugha inavyotumika, katika mafumbo ambayo maana yake ya ndani imefichika mafumbo huundwa na wahusika na fani yake. Mfano yule anayetoa fumbo (anasema fumbo mfumbie mjinga ) Yule anayejibu (mwerevu ataling’amua) hapa anamainisha mjinga hawezi akalifumbua fumbo ila mwerevu hulifumbua pia mjinga anaweza akadanganywa ila mwerevu hawezi kudanganywa. Fumbo hili linahamasisha mtu afanye juhudi katika mambo ili afanikiwe kama mwerevu.
Lakabu ni majina ya kupanga ambayo baadhi ya watu hupewa au kujipatia kutokana na sifa zao za kimwili, kinasaba, kitabia au kimatendo. Majina haya huwa ni sitiari. Majina haya huweza kumsifia mtu au kumkosoa. Mfano Mkuki uwakao – Jomo Kenyatta,Sakarani – mlevi, Simba wa yuda – Haile sellasie.
Katika kigezo cha umbile na tabia inayohusika Mulokozi ameonyesha lakabu hutumia maneno yenye maana iliyofungwa na sitiari, pia lakabu huwa na wahusika yule anayepewa sifa. Mfano mkuki uwakao – Jomo Kenyatta na anayetoa sifa.
Katika muktadha na namna ya uwasilishaji lakabu huwa na dhima mbalimbali kama kusifia, mfano baba wa taifa, inatoa sifa ya utendaji bora wa kazi, simba wa yuda inaonyesha mshupavu. Mkuki uwakao inaonyesha kiongozi  mchapa kazi. Pia lakabu hukosoa na kuonya mfano sakarani- ulevi hapa inaonyesha kuwa mtu mlevi hafai katika jamii. Lakabu huwa na matini yanayobadilika, hivyo ni sanaa inayopita, lakabu hufuata watu wakati na mahali.
Ushairi, ni sanaa ya vina inayopambanuliwa kama nyimbo mashairi na tenzi. Zaidi ya kuw na vina ushairi una ufasaha wa kuwa na maneno machache au muhtasari mawazo na maono ya ushairi huvuta moyo kwa namna ya ajabu. Mulokozi (1989) anasema ushairi hupambanuliwa na lugha ya kawaida kwa kutumia lugha na mbinu za kimuktadha. Kauli za kishairi hupangwa kwa kufuata wizani maalumu na mawimbi ya sauti na mara nyingi lugha ya mkato na mafumbo hutumika ushairi una fani zinazoambatana na muziki wa ala na wakati mwingine hupata wizani wake kutokana na mapigo ya muziki huo wa ala. Mulokozi (1989) amegawa ushairi katika mafungu mawili ambayo ni nyimbo na uwasilishaji.
Nyimbo ni kila kinachoimbwa hivyo hii ni dhana panainayojumuisha tanzu nyingi za kinathari kama vile hadithi huweza katika kundi la nyimbo pindi zinapoimbwa . Vipera  vya nyimbo ni tumbuizo, bembea, kongozi, nyimbo za dini, tenzi, tendi, mbolezi, kimai, nyiso, nyimbo za vita, nyimbo za uwindaji, nyimbo za taifa, nyimbo za watoto na nyimbo za kazi.
Katika kuainisha tanzu hiii ya nyimbo Mulokozi  ametumia vigezo vyote viwili, tukianza na kigezo cha kwanza ambacho ni umbile na tabia ya kazi inayohusika Mulokozi ameonyesha jinsi vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa na kuipa mwelekeo. Vipengele vilivyo katika nyimbo ni namna lugha inavyotumika .
Mfano: nyimbo za maombolezo hutumia lugha za maombolezo yenye maneno ya  Kufariji  tofauti na nyimbo za sherehe huwa na lugha ya furaha na  kuchangamsha.
Katika kigezo hiki pia cha umbile na tabia ya kazi inayohusika Mulokozi ameonyesha muundo wa fani na wahusika katika nyimbo. Mfano: mambo muhimu yanayotambulisha nyimbo ( fani ya nyimbo) Muziki wa sauti ya muimbaji au waimbaji( wahusika), Muziki wa ala (kama ipo), Matini au maneno yanayoimbwa,Hadhira inayoimbiwa,Muktadha unaofungamana na wimbo huo mfano sherehe, ibada na kilio.
Pia Mulokozi katika kuainisha tanzu ya nyimbo ametumia kigezo cha pili yaani muktadha na namna ya uwasilishwaji wake kwa hadhira katika kuainisha tanzu hii ya nyimbo amezingatia wakati, watu (wahusika) na mahali. Pia nyimbo ina matini yanayobadilika, yasiyofungiwa katika umbo maalumu yaani ni sanaa inayopita.
Mfano: kuna nyimbo zinazoimbwa kwa kufuata wakati wake, mahali mahususi, na mahali maalumu, mfano wawe na vave hizi ni nyimbo za kilimo, mbolezi hizi ni nyimbo za kilio au maombolezi. Mbolezi huimbwa wakati maalumu, na waombolezaji ambao ni watu( wahusika) na mahali maalumu (mfano msibani)
Maghani ni ushairi unaotolewa kwa kalima badala ya kuimbwa. Zipo maghani za aina mbili, kuna maghani ya kawaida, ambayo huundwa na fani mbalimbali za ushairi simulizi mfano mapenzi, siasa, maombolezo, kazi za dini na kadhalika. Maghani ya masimulizi hutambwa ili kusimulia hadithi, historia au matukio fulani ambayo huambatana na nyimbo. Tanzu za maghani ni sifo, vivugo, tondozi, rara, ngano na tendi.
 Maghani ni tanzu iliyoanishwa kwa kutumia kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishwaji wake kwa hadhira. Molokozi ameonyesha maghani huwasilishwa kwa kalima badala ya kuimba, pia dhima za maghani ni kufikisha ujumbe kwa hadhira kwa kuzingatia matukio
Mfano uhuru  kesi za mauaji
Mulokozi anasema maghani huundwa na fani mbalimbali za ushairi simulizi mfano mapenzi, siasa, maombolezo, kazi na dini. Zifuatazo ni fani za ushairi simulizi ambazo ni, Masimulizi hutolewa kishairi, huhusu matukio muhimu ya kihistoria au jamii, huelezea habari za ushujaa na mashujaa, huwasilishwa kwa kughanwa (ala ya muziki), hutungwa papo kwa papo.
Pia maghani huwa na wahusika, na huambatana na muziki wa ala. Mulokozi anasema mutambaji wa ghani hizi huitwa Yeli au Manju na kwa kawaida huwa ni bingwa wa kupiga ala fulani ya muziki (mtambaji huyu ndiye mhusika mkuu)
Maigizo, (drama) ni sanaa inayotumia watendaji kuiga tabia au matendo ya watu na viumbe wengine ili kiburudisha na kutoa ujumbe fulani. Maigizo ni sanaa inayopatikana katika makabila mengi. Mulokozi anasema drama (maigizo) ya kiafrika huambatana na ngoma mtambaji wa hadithi au matendo ya kimila. Kwa  mfano jando na unyago , yapo maigizo yanayofungana na michezo ya watoto, uwindaji , kilimo, na kadhalika. Drama hutumia maleba maalumu kama vizuizui (mask).
Katika kuainisha tanzu hii mulokozi ametumia vigezo viwili,kwa kuanza na kigezo cha kwanza Mlokozi ameainisha,mambo na vipengele vinavyopatikana ndani ya maigizo ambavyo ni maigizo yanayohusu matendo ya kimilana michezo ya watoto,matanga, uwindaji, kilimo na nyinginezo.
Kwa msingi wa umbile na tabia inyohusika vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa na kuipa muelekeo tanzu hii ya maigizo ni lugha inavyotumika katika kuigiza fani na wahusika mfano wahusika wa maigizo wapo na hawa ndio watendaji wakuu katika kufikisha ujumbe. Maigizo hutumia lugha mfano lugha ya kejeli na hata lugha rasmi pia maigizo huwa na fani inayotendwa.
Mulokozi Pia katika kuainisha tanzu hii ya maigizo ametumia kigezo cha pili kinachozingatia muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira, maigizo ni sanaa inayopita isiyofungiwa kaika umbo maalum wala matini yasiyobadilika ila maigizo hubadilika kutokana na tukio linaloigigwa na kuzingatia wakati, watu na mahali mfano maigizo huhitaji sehemu maalumu (jukwaa au uwanja wa kutendea) , wahusika ambao ndio waigizaji wakuu na pia maigizo huenda na wakati.
Ngomezi ni midundo Fulani ya ngoma kuwakilisha kauli Fulani katika lugha ya kabila hilo. Mara nyingi kauli hizo huwa ni za kishairi au kimafumbo
Mulokozi ametumia vigezo vyote viwili katika kuainisha tanzu hii, kwa kuanza na umbile na tabia ya kazi inayohusika ameangalia vipengele ndani vinavyoiumba sanaa na kuipa mielekeo na mienendo ulionao.Vipengele hivyo ni namna lugha inayotumika, kishairi, kinathari, kimafumbo, kiwimbo au kighani. Mfano, katika ngomezi hutumia lugha na kauli za kishairi au kimafumbo.
Pia kigezo hiki huangalia fani na wahusika kama wapo, katika ngomezi huwa na wahusika ambao hupiga na kuandaa ngoma hizo.hii hujionyesha katika  utofauti wa upigaji wa ngoma hizi kutokana lengo lake  ambapo inaweza kutoa taarifa, tahadhari au ngomezi za uhusiano.
Katika kigezo cha pili muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira Mulokozi ameonyesha jinsi ngomezi ilivyo ni sanaa ambayo huandaliwa kwa matukio maalum. Pia ngomezi hutawaliwa na vitu vitatu muhimu katika kigezo hiki ambavyo ni watu, wakati na mahali.
M.M Mulokozi katika mulika amejitahidi kuelezea na kuzigawa tanzu na vipera vya fasihi simulizi kwa kuzingatia vigezo vyote viwili, yaani umbile na tabia ya kazi inayohusika na kigezo cha muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira.
Pamoja na kujitahidi huko, kuna baadhi ya mapungufu ambayo yamejitokeza kama;
Mulokozi ameonyesha utenzi wa ngomezi, ila hajayuonyesha vipera au vitanzu vinavyojitokeza au kupatikana katika utanzu huu.
Mulokozi ameainisha na vipera vya fasihi simulizi lakini yeye mwenyewe anakiri kuwa bado hakuna wataalamu walioshughulikia suala hili undani zaidi kwani tanzu za fasihi simulizi hutifautiana kati ya jamii na jamii, Hivyo Mulokozi ameonyesha udhaifu wa kitaaluma
Mulokozi ameshindwa kutofautisha istilahi ya Tanzu na Vipera. Badala ya kutumia vipera yeye ametumia tanzu: vipera vya hadithi yeye anasema fungu au tanzu za kihadithi.
Mulokozi pia ameonyesha udhaifu pale anaposema misimu ikipata mashiko huingia kwenye methali, wakati misimu ikipata mashiko ya kutosha si lazima kuingizwa kwenye methali tu bali huingizwa kwenye msamiati wa lugha sanifu mfano: ngunguli, ngangali na ulanguzi
Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kuwa, uainishaji wa tanzu na vipera vya fasihi simulizi kama vilivyoainishwa na Mulokozi vinaingiliana kifani na  kimaudhui.
KIELELEZO KINACHOONYESHA TANZU NA VIPERA VYA FASIHI SIMULIZI.

1 comment: